habari

MATANGAO

Tuesday, September 18, 2012

Mkutano wa viongozi wa vilabu vya ligi kuu ya Tanzania bara uliofanyika leo jioni umemalizika na kutoa maamuzi ya pamoja kwamba vilabu hivyo hivyo vinavyoshiriki ligi kuu ya msimu huu haviutambui mkataba wa udhamini wa ligi uliosaniwa na Katibu mkuu wa shirikisho la soka nchini Bwana Angetile Osiah.
Katika mkutano huo ambao uliudhuriwa na takribani viongozi waote wakuu wa vilabu, umeamua kuchukua maamuzi ya kutoutambua mkataba huo na pia wameamua kwamba ndani ya siku 7 zijazo watakutana na kampuni yasimu ya Vodacom kwa ajili ya kujadili upya mkataba wa udhamini wa ligi kuu.

Vilabu pia kwa kauli ya pamoja wameagiza kwamba Katibu mkuu wa TFF, Angetile Osiah awaandikie barua kampuni ya ya Zantel ambao ndio wadhamini wa klabu ya African Lyon kwamba mkataba wao wa udhamini usimamishwe kwa kipindi cha siku saba ili kuweza kuweka mambo sawa .

Kwa maana siku saba zijazo kuanzia Jumatano ya leo, umoja wa vilabu hivyo vitatoa tamko rasmi juu ya masuala yote ya udhamini wa ligi kuu na namna jinsi suala la udhamini wa Zantel kwa African Lyon utakavyokuwa.

Pia katika hatua nyingine kumekuwepo na taarifa kwamba Mwenyekti wa kamati ya mchakato wa kuunda kampuni ya ligi kuu, makamu Mwenyekiti wa Simba Godfrey Nyange Kaburu ataondolewa katika nafasi hiyo kutokana na tuhuma za kutokuwa na umoja na viongozi wenzie wa vilabu katika kupigania maslahi ya vilabu vyote.


Mtu anayepewa nafasi ya kuchukua nafasi ya Kaburu ni makamu mwenyekiti wa Yanga Clement Sanga.

Michuano ya Ligi Kuu ya Vodacom kuwania ubingwa wa Tanzania Bara inaingia raundi ya pili kesho (Septemba 19, 2012) kwa timu zote 14 kuumana katika viwanja saba tofauti nchini.
 
Wakati Simba ikiwa mgeni wa JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Mtibwa Sugar itakuwa mwenyeji wa Yanga kwenye Uwanja wa Jamhuri, mjini Morogoro.
 
Viingilio kwa mechi ya Uwanja wa Taifa vitakuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 wakati kwenye Uwanja wa Jamhuri itakuwa sh. 3,000 kwa sh. 10,000.
 
Mechi nyingine za ligi hiyo zitakazochezwa kesho ni African Lyon vs Polisi Morogoro kwenye Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam. Nayo Ruvu Shooting itashuka kwenye Uwanja  wake wa Mabatini, Mlandizi kuikabili Mgambo Shooting kutoka Handeni mkoani Tanga.
 
Tanzania Prisons itakuwa kwenye Uwanja wake wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya kuisubiri Coastal Union ya Tanga wakati Oljoro JKT itaitembelea Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba. Uwanja wa CCM Kirumba, jijini Mwanza utashuhudia mechi kati ya wenyeji Toto Africans na Azam.
 

Monday, September 17, 2012


AZAM FC tayari wako mjini Mwanza na asubuhi hii wanafanya mazoezi kwenye Uwanja wa Chuo cha Ualimu (TTC), Butimba mjini humo kujiandaa na mechi yao ya pili ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya wenyeji Toto African, Uwanja wa Kirumba mjini humo.
Azam iliyoanza vema ligi hiyo kwa ushindi wa 1-0 kwenye Uwanja wa Kaitaba, Bukoba, bao pekee la Abdulhalim Humud dhidi ya wenyeji Kagera Sugar, imepania kuondoka na pointi zote sita katika mechi zake zote mbili za Kanda ya Ziwa.
Aidha, mabingwa hao wa Kombe la Mapinduzi kesho watafanya mazoezi kwenye Uwanja Kirumba, ili kuuzoea kabla ya mchezo wa keshokutwa, ambao unatarajiwa kuwa mkali na wa kusisimua.
Toto Africans itahitaji ushindi kwenye mchezo huo, ili kurejesha imani kwa mashabiki wake baada ya kulazimishwa sare ya 1-1 na JKT Oljoro, katika mchezo wa ufunguzi Jumamosi.
Kuelekea mchezo huo, Mserbia anayeinoa Azam, Boris Bunjak ameomba marefa wachezeshe kwa haki, kwani anaamini vijana wake wanaweza kushinda pale tu sheria 17 zinapotekelezwa uwanjani na si vinginevyo.
Kocha huyo aliwalalamikiwa marefa waliochezesha mechi yao ya Ngao ya Jamii na Simba kwamba waliwabeba mno wapinzani wake, hata wakatoka nyuma kwa 2-0 na kushinda 3-2.
Kwa upande wake, Kocha wa Toto, John Tegete amesema kwamba baada ya kulazimishwa sare na Oljoro, Jumatano watapigana kufa na kupona ili kushinda mechi ya kwanza ya Ligi  Kuu.
“Sare ya juzi kwa kweli hatukuitarajia, tulicheza vizuri, tulipata nafasi nyingi tukapoteza, lakini kwa siku mbili hizi tutafanyia kazi makosa yetu na Jumatano tunaomba mashabiki waje kwa wingi kushuhudia mabadiliko, tunawaahidi ushindi,”alisema baba huyo wa mshambuliaji wa Yanga, Jerry Tegete. 

KOCHA Mkuu wa Yanga, Mbelgiji Tom Saintfiet amewaomba radhi mashabiki wa Yanga kwa sare ya Jumamosi kwenye Uwanja wa Sokoine na amesema kesho anapeleka wachezaji 18 Morogoro kwa ajili ya mechi ya pili ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Mtibwa Sugar, akiwa ana matumaini makubwa ya ushindi.
Saintfiet ameiambia http://ramadhanabubakar.blogspot.com/ leo kwamba sababu nyingi zilichangia Yanga kutocheza kwa ubora wake Mbeya, ikiwemo hoteli mbaya na chakula kibaya na kwa ujumla alisema hawakuwa vizuri kabla ya mechi hiyo.
“Mimi kwa mfano sijaoga siku mbili, kwa kweli tulikuwa katika mazingira magumu na wapinzani wetu walicheza soka ya kuudhi tangu mwanzo, kupoteza muda, na marefa hawakuchukua hatua, tulipoteza nafasi kupitia kwa Kiiza (Hamisi) na Msuva (Simon), siwezi kulaumu mchezaji wangu yeyote, lakini hiyo ndiyo hali halisi,”alisema Saintfiet.
Alisema kesho asubuhi timu itafanya mazoezi kwenye Uwanja wa sekondari ya Loyola, Mabibo, Dar es Salaam na saa 8:00 mchana watasafiri kwa njia ya barabaraba kwenda Morogoro ambako wakifika watatafuta hoteli nzuri mapema.
Alisema anajua hata Uwanja wa huko, Jamhuri si mzuri na mechi itakuwa ngumu kwa sababu Mtibwa Sugar nao walitoka sare ya bila kufungana na Polisi katika mchezo wao wa kwanza Jumamosi na anaiheshimu timu hiyo kama moja ya timu tano kubwa Tanzania, pamoja na Simba, Azam na Coastal Union.
“Lakini pamoja na kwamba Simba wamependelewa kupangiwa ratiba ya kuanza kucheza nyumbani mechi tano mfululiuzo, nakuambia Mei mwaka 2013 Yanga ndio itavishwa taji la ubingwa wa Ligi Kuu, acha wafurahie sasa hivi, watalia mwisho,”alisema Mtakatifu Tom.
Kuhusu wachezaji 18 anaokwenda nao Morogoro, Mtakatifu Tom alisema atawataja baada ya mazoezi ya kesho na hiyo inaonekana ni kwa sababu ya kufuatilia hali za wachezaji ambao kwa sasa hawako vizuri, akiwemo kiungo Haruna Niyonzima.
Wachezaji aliokwenda nao Mbeya walikuwa ni makipa; Yaw Berko, Ally Mustafa ‘Barthez’, mabeki Shadrack Nsajigwa, Juma abdul, Godfrey Taita, Mbuyu Twite, Kevin Yondan, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, David Luhende, Oscar Joshua na Stefano Mwasyika.
Aliwataja viungo ni Athumani Iddi ‘Chuji’, Haruna Niyonzima, Frank Domayo, Rashid Gumbo, Nizar khalfan, Shamte Ally na Simon Msuva, wakati washambuliaji ni Jerry Tegete, Didier Kavumbangu, Said Bahanuzi na Hamisi Kiiza, wakati waliobaki walikuwa ni kipa Said Mohamed, mabeki Ladislaus Mbogo, Job Ibrahim, viungo Juma Seif ‘Kijiko’, Salum Telela, Omega Seme, Nurdin Bakari, Idrisa Assega na Issa Ngao wa Yanga B, anayekomazwa kikosi cha kwanza.

UCHAGUZI WA WANACHAMA WA TFF
Kamati ya Uchaguzi ya TFF katika kikao chake kilichofanyika Septemba 15, 2012 ilijadili michakato ya uchaguzi wa vyama wanachama wa TFF inayoendelea hivi sasa kabla ya kufanyika Uchaguzi Mkuu wa TFF mwishoni mwa mwaka huu. Kamati iliamua yafuatayo;

Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Njombe (NJOREFA)
Kamati ya Uchaguzi ya TFF ilibaini kuwa uongozi wa muda wa NJOREFA haukutoa ushirikiano wa kutosha kuiwezesha Kamati ya Uchaguzi ya NJOREFA kuanza mchakato wa uchaguzi kwa tarehe kwa tarehe iliyokuwa imepangwa na hivyo kusababisha kuchelewa kuanza kwa mchakato huo wa uchaguzi wa mkoa huo mpya.

Kamati imebaini pia kuwa kutokana na changamoto za kiuongozi zinazoukabili mkoa huo mpya, mchakato wa uchaguzi ulioanza Septemba 2, 2012 haukuzingatia kikamilifu Kanuni za Uchaguzi za Wanachama wa TFF.

Kutokana na kasoro hizo za msingi, mchakato wa uchaguzi wa NJOREFA utaanza upya Septemba 18, 2012 ukizingatia Kanuni za Uchaguzi za Wanachama wa TFF. Uchaguzi wa NJOREFA utafanyika Oktoba 28, 2012.

Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Tabora (TAREFA)
Kamati ilibaini kuwa kuna mkanganyiko katika mchakato wa uchaguzi wa TAREFA na kwamba mkanganyiko uliotokea umesababishwa na Kamati ya Uchaguzi ya TAREFA kutotimiza wajibu wake wa kusimamia uchaguzi wa TAREFA kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi za Wanachama wa TFF.

Kutokana na kuvurugika kwa mchakato wa uchaguzi wa TAREFA uliosababishwa na kiwango kikubwa cha ukiukwaji wa Kanuni za Uchaguzi, Kamati ya Uchaguzi ya TFF imejiridhisha kuwa Kamati ya Uchaguzi ya TAREFA haina uwezo wa kusimamia majukumu ya uchaguzi wa TAREFA na kuzingatia kikamilifu matakwa ya Kanuni za Uchaguzi ya Wanachama wa TFF.

Kwa kuwa Kamati ya Uchaguzi wa TAREFA imeshindwa kutimiza wajibu wake na hivyo kusababisha mkanganyiko na uvurugaji wa uchaguzi wa TAREFA, Kamati ya Uchaguzi ya TFF kwa mamlaka yake yaliyoainishwa katika Katiba ya TFF Ibara ya 49(1) na Kanuni za Uchaguzi za Wanachama wa TFF Ibara ya 10(6), 26(2) na (3) imeamua yafuatayo;

(i) Imefuta Kamati ya Uchaguzi ya TAREFA. Uongozi wa TAREFA unatakiwa kuteua Kamati mpya ya Uchaguzi itakayoandaa na kutekeleza majukumu yake ikizingatia Kanuni za Uchaguzi za Wanachama wa TFF na Katiba ya TAREFA. Uteuzi wa Kamati mpya ya Uchaguzi ya TAREFA ufanyike kabla ya Septemba 24, 2012.

(ii) Imefuta mchakato wa uchaguzi wa TAREFA. Mchakato wa uchaguzi utaanza upya Septemba 25, 2012 na uchaguzi utafanyika Novemba 4, 2012.

Vyama vya Mpira wa Miguu mikoa ya Manyara (MARFA) na Kilimanjaro (KRFA)
Uchaguzi wa MARFA na KRFA utafanyika Septemba 22, 2012 kama ilivyopangwa.

UTENDAJI WA KAMATI ZA UCHAGUZI ZA WANACHAMA WA TFF
Kamati imebaini baadhi ya viongozi wa vyama vya wanachama wa TFF wanaomaliza muda wao wanashiriki kudhoofisha michakato ya uchaguzi ya vyama vya mpira wa miguu kwa kutotoa fursa kwa Kamati za Uchaguzi za vyama wanachama kuanza michakato ya uchaguzi kwa tarehe zilizopangwa na Kamati ya Uchaguzi ya TFF.

Kwa kuwa ni wajibu wa viongozi waliopo madarakani kuhakikisha kuwa vyama vyao vinafanya uchaguzi kwa mujibu wa Katiba zao na Kanuni za Uchaguzi, Kamati ya Uchaguzi ya TFF haitasita kupendekeza kwa Mamlaka husika za TFF vyama hivyo kuchukuliwa hatua za Kikatiba kwa kushindwa kutimiza matakwa ya Katiba ya TFF kwa kuwa na uongozi ambao muda wa ukomo wa madaraka utakuwa umepita na hivyo kutokidhi matakwa ya Ibara ya 12(2)(a) ya Katiba ya TFF.

Kamati ya Uchaguzi ya TFF inavishauri vyama wanachama wa TFF kuzingatia ratiba ya uchaguzi na Kanuni za Uchaguzi za Wanachama wa TFF wakati wote wa michakato ya uchaguzi wa viongozi wa vyama vyao. Viongozi walioko madarakani wanatakiwa kutoa ushirikiano kwa Kamati za Uchaguzi kama ilivyoianishwa kwenye Kanuni za Uchaguzi.

Hamidu Mbwezeleni
Makamu Mwenyekiti kamati ya uchaguzi
Siku ya jumamosi tarehe 15, mwezi wa tisa mwaka 2012, soka la Tanzania lilitengeneza historia nyingine mbaya.
Ilikuwa ni siku ya ufunguzi wa ligi kuu ya soka ya Tanzania bara na timu mbalimbali zilikuwa viwanjani kutupa karata zao za mwanzo kabisa ndani ya msimu mpya wa 2012/13. Miongoni mwa mechi zilizokuwa zichezwe siku hiyo ilikuwa ni mechi kati mabingwa watetezi Simba na African Lyon zote kutoka Jijini Dar es Salaam.

Mapema asubuhi ya siku hiyo kulikuwa na mkutano wa waaandishi wa habari ulioitishwa na African Lyon na kampuni ya mawasiliano ya  simu za mkononi ya Zantel ambao siku hiyo walikuwa wameamua kutangaza rasmi muunganiko wao wa kibiashara - ambapo klabu hiyo itakuwa ikidhaminiwa na Zantel kwa muda wa miaka mitatu.

Hii ilikuwa habari nzuri kwa wapenda maendeleo ya soka wa Tanzania ikizingatiwa ni vilabu vichache tu ndivyo ambavyo vilikuwa vina udhamini hivyo kuwa na nguvu kuliko vilabu vingine na mwisho wa siku ushindani wenye tija katika kuukuza mpira ukawa sio mkubwa. Hivyo kuingia kwa Zantel kuidhamini African Lyon kulimaanisha kutaipa nguvu klabu hiyo kuweza kupambana na vilabu vingine vyenye fedha na nguvu kama Simba, Yanga, Azam, Mtibwa na nyinginezo.

Muda ukapita na saa ya kwenda uwanjani ikafika, timu zote zikawasili uwanjani na kuanza maandalizi ya mchezo. Kama ilivyo ada, kutokana udhamini ulivyo Simba ambao udhaminiwa na Bia ya Kilimanjaro walikuwa na jezi zao zenye nembo ya mdhamini wao na wakaenda kuweka mabango yao ya mdhamini wao pembeni mwa uwanja - African Lyon nao baada ya kuwa wameshakamilisha udhamini wa Zantel, walikuwa na jezi zao zenye nembo ya mdhamini wao na pia wakaenda kuweka mabango uwanjani kama ilivyokuwa kwa Simba. Lakini cha ajabu ikatolewa amri kutoka TFF kwamba African Lyon hawatoruhusiwa kuvaa jezi za mdhamini wao mpya na mabango yao yakatolewa dimbani - huku sababu ikitoka kwamba hairuhusiwi kwa timu binafsi inayoshiriki ligi kuu kuwa na udhamini wa kampuni ya simu tofauti na Vodacom ambao ndio wadhamini wakuu wa ligi kuu. Kwa maana hiyo African Lyon iliwabidi watafute jezi nyingine zisizo na nembo ya mdhamini wao mpya na mabango yao yote yakatolewa ndani ya uwanja wa taifa.

Kitendo kile hakikuwa kizuri na kilitishia hata mechi kuvunjika kwa sababu viongozi wa  African Lyon wanasema walifanya kila kitu kwa kufuta sheria na kanuni hivyo walikuwa sahihi, na walisisitiza hata katika kikao cha kabla ya mechi walipeleka jezi zao na zikapitishwa na kwa ajili ya kuchezewa katika mechi ya baadae.

Kiukweli kitendo kile ambacho kilikosa majibu ya kueleweka hakikuwa kizuri na kileleta aibu katika soka letu, pia kinaweza  kuwakimbiza wadhamini wengine ambao walikuwa na interest ya kuja kuwekeza kwenye soka letu.

BAADA YA MECHI
Kutokana na kitendo kile nilijaribu kufuatiliwa na kutaka kujua kiundani kwanini imekuwa tatizo kwa African Lyon kuwa na mdhamini ambaye ni mshindani wa kibiashara na mdhamini mkuu wa ligi.

Katika kufuatiliwa kwangu nimekuja kupata taarifa za kuaminika kutoka baadhi ya viongozi wakuu wa vilabu vya ligi kuu kwamba mpaka sasa hakuna mkataba wowote halali wa kibiashara baina ya vilabu hivyo na kampuni yoyote juu ya udhamini wa ligi kuu ya Tanzania bara ambayo msimu huu ipo chini ya vilabu kupitia kamati ya ligi. Kwa maana katibu mkuu wa TFF Bwana Angetile Osiah amekuwa akitoa taarifa za uongo juu ya udhamini mpya wa Vodacom kwenye ligi kuu.

Ni kweli kwamba kumekuwepo au kulikuwepo na mazungumzo ya kati ya Vodacom na vilabu kupitia mwakilishi wao TFF, lakini mpaka sasa hakuna mkataba wa kisheria ulio halali baina ya pande mbili kwa maana hiyo ligi haina mdhamini rasmi. Hivyo taarifa anazotoa katibu mkuu wa TFF sio sahihi.

Mkataba huo sio halali kwa kuwa hakuna kiongozi wa timu yoyote aliyesaini mkataba huo wa udhamini na Vodacom. Ukweli ni kwamba TFF kupitia Angetile Osiah alikuwa kama mdhamini(Guarantor) katika majadiliano na utiaji saini wa mkataba, hivyo ilipaswa kwanza viongozi wa vilabu kupitia viongozi wao Mzee Said Mohamed na Wallace Karia wasaini kwanza ndio wampe Guarantor wao TFF aweke saini, lakini haikuwa hivyo na kwasababu wazijuazo wenyewe Angetile Osiah akatia saini kwenye mkataba kabla ya vilabu kufanya hivyo.

Je kwa sababu zipi, mdhamini wa kwenye mkataba akawa na haraka ya kuusaini mkataba kuliko wahusika halisi kabisa ambao ni vilabu au kuna 10% ya kuhakikisha dili la udhamini linaenda pale anapopataka? Majibu anayo mwenyewe.

KWANINI VILABU HAVIJASAINI MKATABA MPYA NA MDHAMINI WA LIGI?
Viongozi wakuu wa vilabu wanasema sababu kuu walizoshindwana mpaka sasa na mdhamini wa ligi aliyepita ni tatu tu.

1: Mdhamini kutaka apate upekee - yaani asiyewepo mpinzani wa moja kwa moja wa kibiashara katika issue nzima ya kutoa udhamini katika ligi, kwa shirikisho na vilabu pia. Vilabu vikatoa kauli ya pamoja kwamba ili mdhamini mkuu aweze kupata haki ya upekee inabidi a-double fedha anayota kwa  mwaka, jambo ambalo Vodacom walilikataa.

2: Fedha za udhamini: Kwa mujibu wa viongozi wa vilabu ni kwamba mdhamini wa ligi aliyepita alitoa ofa ya kutoa kiasi cha Billioni 1.6 kwa kila mwaka ndani ya kipindi cha miaka 3, lakini viongozi wa vilabu wakalipinga hilo kwa kutoa sababu kwamba lazima kiwepo kipengele cha ongezeko la thamaini ya fedha - kwa maana shilingi billioni ya mwaka huu haitakuwa sawa na thamani ya mwaka au miaka miwili mbele. Kwa maana hiyo wakaomba liwepo ongezeko la asilimia 10 ya fedha wanayopewa kwa kila mwaka.

3: Pendekezo la tatu ni kwamba mkataba uwe wa miaka miwili na si mitatu. Suala hili pia  likakataliwa.

Mapendekezo haya matatu ndio yaliyochangia uchelewashaji au kutokuwepo kwa mkataba wa udhamini wa ligi ulio halali kisheria.

NINI KINAFUATA
Kwa taarifa nilinazo ni kwamba viongozi wa timu za ligi kuu walikuatana jana jioni jijini Dar Es Salaam ili kujadili namna ya kuepukana na ukiritimba wa TFF na mikataba yao, na ikiwa kutatokea kampuni yoyote yenye  kutaka kuidhamini ligi kuu lazima suala ya 'exclusivity ' lisiwepo ama kuongeza kiasi cha pesa na kufikia walau shilingi za kitanzania bilioni tatu ili kuondoa aibu ambayo iliikumba soka ya Tanzania jumamosi.

Pia wakaafikiana kwamba ligi ya mwaka huu itaitwa "Ligi kuu ya Tanzania Bara" na sio vinginevyo, huku wakitoa kauli rasmi kwamba hawautambui mkataba wa udhamini na Vodacom kwa sababu sio halali kwa maana hakuna kiongozi yoyote wa klabu aliyetia saini mkataba huo.

Pia viongozi wa vilabu kwa pamoja wamesikitishwa sana na kitendo ilichofanyiwa African Lyon na kukilaani vikali.